Enjoy the Swahili poem about the State of Youth in Tanzania (Haya ndo maendeleo ya vijana)

Ninamshukuru jalali, kunijalia uhai,

Na hii bora hali, shetani kwangu hakai

Bada ya hii kauli, na ninyi nawasabai

Haya ndo maendeleo, ya vijana Tanzania

Baada ya hizo salamu, sasa zafuata pongezi

Restilesi ndo muhimu, hali kuiweka wazi

N a washirika muhimu, walofanikisha kazi

Haya ndo maendeleo, ya vijana Tanzania

Katika mikoa saba, kaziyo imefanyika

Hakikuachwa kibaba, haliyo imefichuka

Tumezimaliza raba, mitaani kuzunguka

Haya ndo maendeleo, ya vijana Tanzania

Kuhusu wao uchumi,  vijana wamefunguka

Bila kuminya ulimi, baadhi wachakarika

Kilimo hawakilimi, malipo si uhakika

Haya ndo maendeleo, ya vijana Tanzania

Juu ya wao uzazi, haki zao hawajui

Hawashiriki uzazi, manesi ni maadui

Mipango haiku wazi, hatima hawaijui

Haya ndo maendeleo, ya vijana Tanzania

Ushiriki mitaani, ni wachache wako mbele

Mifumo serikalini, waipigia kelele

Hawawekwi shirikani, kupewa kipaumbele

Haya ndo maendeleo, ya vijana Tanzania

Lipo hili babalao, la kuitunga katiba

Namna ushiriki wao, wanahitaji tiba

Washangaa tume yao, maoni inavyoiba

Haya ndo maendeleo, ya vijana Tanzania

Kwa uchaguzi ujao, wengi wataka shiriki

Kwa huo wao upeo, wadai ni yao haki

Mawio hata machweo, mafisadi hawataki

Haya ndo maendeleo, ya vijana Tanzania

Yapo mengi ya muhimu, ripoti itaeleza

Wapo watu wa muhimu, mwishoni nitaeleza

Keni na Fransi walimu, hadi kazi twamaliza

Haya ndo maendeleo, ya vijana Tanzania

Osca Kefa na Devidi, wao wamo miongoni

Agi Kikoti wazidi, Denisi yu ulingoni

Lau Jaco si wakaidi, Efurahimu makini

Haya ndo maendeleo, ya vijana Tanzania

Kalamu naweka chini, msifikiri frimasoni

Vijanangu komaeni, katu musione soni

Ukataeni uhuni, maendeleo usoni

Haya ndo maendeleo, ya vijana Tanzania

This entry was posted in Uncategorized. Bookmark the permalink.

Leave a comment